Pata Historia ya Wilaya ya Korogwe Hapa
Historia ya Wilaya ya Korogwe
Wilaya ya Korogwe ilianza mwaka 1966
ambapo ilitenganishwa na Wilaya ya Lushoto. Kutokana na Wilaya ya
Lushoto kuwa na eneo kubwa kiutawala, ilikuwa vigumu kutoa huduma kwa
wananchi. Kabla eneo hili halijatengana na Wilaya ya Lushoto
lilijulikana kama Korogwe “Sub-District” na mtawala wa eneo alikuwa ni
“District Officer Incharge”.
Asili ya jina Korogwe ni jina la mmoja
wa wakazi wa awali wa eneo hilo ambaye alijulikana kama Mkorogwe ambaye
alikuwa ni Mzigua kwa kabila aliyeishi katika kitongoji cha Kilole-
Kambi ya Maziwa. Mwaka 1966 Korogwe ilitangazwa kuwa Wilaya kupitia
Tangazo la Serikali Na. 429 la Mwaka 1966 (GN No.429 of 1966). Mkuu wa
Wilaya wa kwanza aliitwa Rajabu Semvua, wakati huo ilikuwa na Tarafa nne
(4) ambazo ni Korogwe, Mombo, Bungu na Magoma kwa kuzingatia mfumo wa
Kichifu uliokuwepo kabla ya Uhuru.
Kufuatia Tangazo hilo la Serikali
ilianzishwa Halmashauri kamili iliyojulikana kama Halmashauri ya Wilaya
ya Korogwe. Mtendaji Mkuu wa Halmashauri kwa wakati huo alijulikana
kama Mkurugenzi wa Maendeleo wa Wilaya (District Development
Director- DDD) ambaye alishirikiana na Wakuu wa Idara mbalimbali katika
kufanikisha utendaji kazi wa Ofisi yake. Katika jitahada za kusogeza
huduma karibu na wananchi, Serikali kupitia Tangazo Na. 352 la tarehe
19/7/2004 ilianzisha Halmashauri ya Mji na kuifanya Wilaya ya
Korogwe kuwa na Halmashauri mbili
(Halmashauri ya Mji na Wilaya). Wilaya ina eneo lenye kilomita za mraba
3,756 ambazo zimegawanyika katika Halmashauri ya Mji Korogwe yenye
Kilomita za mraba 212 na Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe yenye Kilomita
3,544. Halmashauri hizi zina Tarafa 5, Kata 28, Vijiji 139,
Vitongoji 610 na Mitaa 17 na zinakadiriwa kuwa na jumla ya watu
324,020.
Wilaya ya Korogwe inapitiwa na barabara
kuu inayoiunganisha na Miji mikubwa ya Dar-es- salaam, Arusha,
Kilimanjaro, Pwani, Tanga Mjini, Morogoro na nchi za jirani ambazo ni
Kenya na Uganda, hii inaifanya Korogwe kuwa Mji wa Kibiashara.
No comments:
Post a Comment